Yanga SC kuivaa Polisi TZ katika michuano ya Azam Sport Federation Cup

KANDANDA Yanga SC kuivaa Polisi TZ katika michuano ya Azam Sport Federation Cup

Na Zahoro Juma • 17:19 - 02.02.2024

Michuano hiyo bingwa wake hucheza Kombe la Shirikisho Afrika

Mabingwa wa tetezi wa michuano ya Azam Sport Federation Cup (ASFC), timu ya Yanga SC, imepangwa kucheza na Polisi Tanzania katika mechi ya mzunguko wa tatu huku watani zao wa jadi, Simba SC wao wakipangwa dhidi ya Mamlaka ya Mapato Mkoa wa Kilimanjaro (TRA).

Simba na Yanga wote watakuwa katika viwanja vya nyumbani katika michezo hiyo ambayo inatarajia kuchezwa kuanzia Februari 19 na 20.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Shirikisho la Mpira wa Miguu (TFF), kwa upande wa Azam, wao wamepangwa nyumbani ambapo watacheza na Green Worriors.

Yanga iliingia katika hatua hiyo baada ya kuwafunga Hausang FC ya mkoani Njombe kwa jumla ya mabao 5-1 huku Simba wao wakiibuka na ushindi wa 4-0 dhidi ya Tembo katika hatua iliyopita.

Mshindi kati ya Yanga na Polisi Tanzania anatarajia kucheza mechi ya ugenini na mshindi kati ya Dodoma Jiji au Biashara United katika hatua ya 16 Bora.

Kwa upande wa mshindi kati ya Simba au TRA Kilimanjaro, atacheza ugenini dhidi ya mshindi kati ya Mashujaa au Mkwajuni.

Ratiba kamili ya 32 Bora/16 Bora

Singida FG / FGA Talents vs Tabora Utd / Nyamongo

Azam / Green Warriors vs Mtibwa / Stand United

Mashujaa / Mkwajuni vs Simba / TRA Kilimanjaro

KMC / Gunners vs Ihefu / Mbuni

Coastal Unioni / Mbeya Kwanza vs JKT Tanzania / TMA

Dodoma Jiji / Biashara United vs Yanga / Polisi Tanzania

Namungo / Transit Camp vs Kagera Sugar / Pamba

Geita Gold / Mbeya City vs Rhino Rangers / Mabao

Tags: