Kocha Simba SC aipiga mkwara Azam FC

Kocha Msaidizi wa timu ya Simba SC, Seleman Matola

KANDANDA Kocha Simba SC aipiga mkwara Azam FC

Na Zahoro Juma • 20:33 - 07.02.2024

Timu hizo zinatarajia kuumana Ijumaa kuanzia saa 10 jioni kwa saa za Afrika Mashariki na Kati katika Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza

Baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 4-0 dhidi ya Tabora United, Kocha Msaidizi wa timu ya Simba SC, Seleman Matola, amesema ushindi huo ni salamu kwa mpinzani anayefuata ambaye ni Azam FC.

Simba Ijumaa itakabaliana na Azam katika 'Dabi ya Mzizima' ambayo inatarajiwa kufanyika Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.

Akizungumza na Pulsesports mara baada ya kukusanya alama tatu, Matola amesema wao kama benchi la ufundi wanajivunia kwa kiwango cha timu yao kwa mechi za hivi karibuni tangu kurejea kwa ligi na wamejipanga kuendelea na mfululizo huo wa matokeo ya ushindi.

"Hizi zinaweza kuwa ni salamu kwa wapinzani wetu ingawa najua mechi yetu ijayo itakuwa ni ngumu sana dhidi ya Azam, hata hivyo kikosi chetu kipo imara na tunajiandaa kwa ajili ya kufanya vizuri," amesema.

Matola pia hakusita kuwamwagia sifa wachezaji wapya ambao wamesajili na Simba kwenye dirisha dogo akidai wana uwezo mkubwa na wana uhakika watawasaidia katika mechi za mashindano mbalimbali.

Ushindi huo ni wa pili mfululizo kwa kikosi cha Simba mara baada ya kushinda kwenye mechi ya Kigoma dhidi ya Mashujaa kwa bao 1-0.

Mechi za hivi karibuni baina ya Simba na Azam, zimekuwa hazitabiriki na hasa msimu uliopita 'wekundu wa Msimbazi' walionekana wateja wa Azam wakifungwa mara mbili na kutoka sare mchezo mmoja katika mechi za michuano yote waliyokutana.