Simba SC yamrudisha Chama kikosini

KANDANDA Simba SC yamrudisha Chama kikosini

Na Zahoro Juma • 18:58 - 02.02.2024

Kiungo huyo wa kimataifa wa Zambia, alisimamishwa kwa utovu wa nidhamu lakini alipata nafasi ya kuliwakilisha taifa lake katika AFCON

Uongozi wa timu ya Simba SC, umemsamehe mchezaji wao, Clatous Chama na kumpa ruhusu ya kusafiri kwenda mkoani Kigoma kuungana na wenzie kwa ajili ya mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya Mashujaa.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo kupitia kurasa zao za mitandao ya kijamii, Chama ameandika maelezo kuhusu shutuma zilizokuwa zinamkabili na baada ya kuzipitia, Kamati ya Ufundi pamoja na Kocha, Abdelhak Benchikha waliamua kumsamehe bila kumpeleka Kamati ya Maadili kama ilivyoelezwa awali.

Chama alisimamishwa mapema Desemba kwa madai ya utovu wa nidhamu akiwa sambamba na mchezaji mwenzake, Nassor Kapama ambaye aliachwa kipindi cha dirisha dogo.

"Uongozi wa Klabu ya Simba unapenda kuwataarifu wanachama na wapenzi wa Simba kuwa umemsamehe mchezaji Clatous Chama," imesomeka taarifa hiyo.

Chama alikuwa nchini Ivory Coast akishiriki michuano ya Afcon akiwa na timu yake ya Taifa ya Zambia ambayo tayari imeshatolewa.

Wachezaji wengine ambao walikuwa wakishiriki Afcon na kutolewa tayari wapo nchini na walijiunga na timu kwenye safari ya Kigoma ambayo ilifanyika jana.

Simba kesho wanakabiliwa na mchezo wa ligi kuu dhidi ya Mashujaa ambao unatarajia kufanyika katika dimba la Lake Tanganyika, Kigoma.

Tags: