Robertinho sasa aigeukia Yanga Jumapili

© Kwa Hisani

KANDANDA Robertinho sasa aigeukia Yanga Jumapili

Zahoro Mlanzi • 13:07 - 30.10.2023

Robertinho amesema mchezo wa 'derby' siku zote huwa ni mgumu na ndio maana anahitaji muda kwa ajili ya kukiandaa kikosi chake ili kufanya vizuri kwenye mchezo huo.

Baada ya kuifunga timu ya Ihefu FC kwenye mchezo wa Ligi Kuu Bara uliofanyika mwishoni mwa wiki, Kocha wa Simba, Roberto Oliveira 'Robertinho', amesema sasa anahitaji kuingia msituni kuwaandalia dozi Yanga.

Ametoa kauli hiyo baada ya kuiongoza timu yake kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 mbele ya Ihefu na kuwiana kwa pointi 18 na Yanga.

Robertinho amesema mchezo wa 'derby' siku zote huwa ni mgumu na ndio maana anahitaji muda kwa ajili ya kukiandaa kikosi chake ili kufanya vizuri kwenye mchezo huo.

Simba wanatarajiwa kuwa wenyeji wa Yanga katika mchezo ujao wa ligi hiyo utakaofanyika Jumapili kwenye Uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam.

Mchezo huo ni muhimu kwa pande zote kutokana na mipango ya kila mmoja kutaka kushinda taji la NBC msimu huu.

"Derby ni mechi ngumu siku zote, hivyo ili kushinda yanahitajika maandalizi ya nguvu na muda wa kutosha," amesema Robertinho.

Akizungumzia kuhusu alama tatu ambazo wamezivuna dhidi ya Ihefu kwa kuwafunga mabao 2-1, kocha huyo, amesema mchezo huo haukuwa mwepesi hasa kwao kutokana na uchovu waliokuwa nao.

Robertinho amesema haikuwa rahisi kwao kutokana na safari mfululizo walizosafiri kwa kipindi kifupi hivyo walikosa muda mzuri wa kupumzisha miili ya wachezaji.

"Wachezaji wangu walikuwa na wakati mgumu na hii imesababishwa na mizunguko yetu ya hivi karibuni, tumefanya safari nyingi lakini bado tumepambana na tumeshinda," amesema.

Robertinho pia amefurahishwa na namna alivyotoa nafasi kwa wachezaji kama Shaban Chilunda, Israel Mwenda na Mosses Phiri na amewapongeza kwa mchango wao uwanjani.

Katika mchezo huo, mabao yao yalifungwa na Jean Baleke kipindi cha kwanza na alitoka nafasi yake ilichukuliwa na Phiri ambaye naye akafunga bao la pili huku bao la Ihefu lilifungwa na Ismail Mgunda.